Svoboda | Graniru | BBC Russia | Golosameriki | Facebook

Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 27, 2024 Local time: 14:31

Watoto watahadharisha tishio la mgogoro wa hali ya hewa duniani kupitia televisheni


Ongezeko la joto nchini Russia ambapo watoto na wazazi wao wakiwa wanaburudika kwa kujimwagia maji.
Ongezeko la joto nchini Russia ambapo watoto na wazazi wao wakiwa wanaburudika kwa kujimwagia maji.

Watazamaji wa televisheni kote duniani watapata ripoti maalum ya hali ya hewa Alhamisi wakati watoto watakapokuwa kwenye televisheni wakitoa utabiri maalum wa hali ya hewa kuhusu mustakabali   wao – tishio la mgogoro wa hali ya hewa.

Kuanzia kwenye CNN mpaka France 2, katika lugha mbalimbali ikiwemo Kihispania, Kiarabu na Kihindu, watoto hao ni sehemu ya juhudi zinazoendeshwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Programu ya Maendeleo (UNDP), Shirika la Kimataifa la Hali ya Hewa (WMO) na Chaneli za Hali ya Hewa.

“Mimi ni Kaylee nikikuletea ripoti maalum kabisa ya hali ya hewa. Kutoka huko, hadi hapa, kila kitu kinachanganya,” Kaylee mwenye umri wa miaka 11 anawaambia watizamaji.

“Siyo tu ripoti ya hali ya hewa kwetu. Ni mustakabali wetu wote,” binti huyo anasema.

Viwango vya Joto Vyaongezeka

Iwapo hali ya hewa inaripotiwa na Kaylee, au Noam au Esteban katika lugha nyingine, ramani ya dunia inaonyesha viwango vya joto mbalimbali vikiendelea kuongezeka.

Huo ni mwanzo tu: inaendelea mbele kwa utabiri kwa mwaka 2050, ulioandaliwa kutokana na matukio ya mioto mbalimbali na kuanguka kwa majumba kufuatia shinikizo la mito inayojaa maji.

Tangazo hilo la dakika moja litapeperushwa katika nchi zaidi ya 80 kupitia vituo mbalimbali na majukwaa ya mtandao wa kijamii mbalimbali.

Utabiri wa Hali ya Hewa katika lugha mbalimbali

Utabiri huo utatangazwa kwa Kifaransa, Kiingereza, Kihispania, Kiarabu, Kihindu, Kiswahili na hata Kithai na Kireno, UNDP ilieleza katika taarifa yake kwa vyombo vya habari.

“Watoto wetu ndiyo watakaokuwa watangazaji wa habari za hali ya hewa siku za usoni, waandishi wa hali ya hewa, wafanyakazi wa dharura na wataalam wa tiba,” alisema muigizaji Nikolaj Coster-Waldau kutoka “Game of Thrones,” mmoja wa mabalozi waanzilishi wa programu hii.

Kampeni hiyo “inatuonyesha sura mbalimbali za wale watakao athirika zaidi na vitendo vyetu vinavyochangia katika hali ya hewa.

Sababu za Kuchukua Hatua

Balozi mwengine, muigizaji Michelle Yeoh, alisema kuwa “wakati ripoti zao za hali ya hewa ni za kufikirika hivi sasa, ni muhimu kwetu kuchukua hatua kabambe kulinda sayari hii kwa ajili ya watoto wetu na vizazi vijavyo.”

Kuna uwezekano mkubwa kuwa mwaka 2024 utashuhudia viwango vya juu vya joto ambavyo havijawahi kuonekana, Wakati Shirika la Kimataifa la Hali ya Hewa limesema mwaka jana lilivunja rekodi “ kuwa na joto kali zaidi ambalo limevunja rekodi ya miaka 10.”

“Maamuzi yetu hivi leo yatatengeneza mustakabali wa vizazi vingi vijavyo. Kampeni hii ni wito wa kuchukua kwa haraka hatua kwa ajili ya usalama wa watu na sayari hii,” Katibu Mkuu wa WMO Celeste Saulo alisema.

Kampeni ya UNDP

Utabiri wa hali ya hewa wa watoto ni muendelezo wa kampeni nyingine ya UNDP iliyozinduliwa mwaka 2021 kujaribu kuhamasisha maamuzi ya hali ya hewa.

Katika kampeni hiyo, dinosaur aliyetengenezwa na kompyuta aliyeitwa Frankie ajitokeza kwa ghafla katika Baraza Kuu la UN akipiga kelele “Angalau tulikuwa na asteroid. Mtatoa udhuru gani?”

“Msichague kuangamia. Waokoeni viumbe kabla ya kuchelewa.”

Forum

XS
SM
MD
LG