Svoboda | Graniru | BBC Russia | Golosameriki | Facebook

Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumapili, Aprili 28, 2024 Local time: 15:58

Hali mbaya ya wakimbizi mpakani mwa Sudan na Sudan Kusini


Wakimbizi kutoka Sudan wakiwa Metema, baada ya kuvuka kwenda Ethiopia, tarehe 2023. Picha na Amanuel Sileshi/AFP.
Wakimbizi kutoka Sudan wakiwa Metema, baada ya kuvuka kwenda Ethiopia, tarehe 2023. Picha na Amanuel Sileshi/AFP.

Rosa Yusif Elias alitoroka Sudan kwa miguu akiwa na watoto wake saba kupitia mpakani kwenda kwenye nchi yake ya Sudan Kusini kwa ajili ya kutafuta usalama.

Lakini hivi sasa yeye na familia yake wamekwama kwa wiki kadhaa katika kambi iliyojitenga na kuelemewa na watu waloikimbia ghasia katika nchi jirani.

Hali ni mbaya katika kambi ya wakimbizi iliyopo karibu na mpakani. Kambi ina watoto wanaokabiliwa na utapiamlo, mivutano inayosababishwa na uhaba wa rasilimali, na familia kulala nje huku idadi ya watu katika kambi hiyo ikiongezeka kila siku.

"Hii sehemu imejaa nzi na nyoka, na chakula siyo kizuri," alisema Elias, ambaye aliikimbia Sudan baada ya mapigano kuzuka kati ya jeshi la serikali na jeshi la RSF tarehe 15 mwezi wa nne.

Alisema watoto wamekuwa wakiharisha. “siku chache zilizopita, watoto watatu wamefariki katika kambi hii."

Msongamano wa wakimbizi unaongezea hali ambayo tayari ilikuwa mbaya huko Sudan Kusini, nchi yenye machafuko inayokabiliwa na vita, njaa na majanga ya asili tangu ipate uhuru kutoka Sudan mwaka 2011.

"Tunateseka katika kambi hii, watoto wanakufa," alisema Santuke Danga, ambaye amekwama kwenye kambi iliyopo jirani na Renk, mji ulioko mpakani ambao umekuwa kitovu cha mzozo huu mpya.

"Tunapanga foleni ili kupata uji kwa ajili ya watoto, kwenye sehemu yanapotoka maji watu hupigana, hakuna usalama na wakati mwingine fisi wanakuja."

Wale wanaowasili wanageukia makundi ya misaada ambayo tayari yanakabiliwa na changamoto yakijaribu kutoa huduma za msingi katika nchi ambayo theluthi mbili ya watu wanategemea msaada wa kibinadamu ili kuishi.

Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi UNHCR linasema zaidi ya watu 100,000 wamevuka kutoka Sudan tangu mapigano yalipoanza takriban miezi miwili iliyopita ikiwa ni wastani wa zaidi ya watu 1,000 kwa siku.

Baadhi yao wanawasili wakiwa wamepanda punda, na wamedhoofika kiasi kwamba hawawezi kuendelea kutembea zaidi.

Forum

XS
SM
MD
LG